Kusoma sura zenye sijda za wajbu katika sala

Page 1

KUSOMA SURA ZENYE SIJDA ZA WAJIBU KATIKA SALA Kimeandikwa na: Shaikh Abdul-Karim al-Bahbahani

Kimetarjumiwa na: Hemedi Lubumba Selemani


ŠHaki ya kunakili imehifadhiwa na: AL-ITRAH FOUNDATION ISBN: 978 - 9987 - 512 - 54 - 6

Kimeandikwa na: Shaikh Abdul-Karim al-Bahbahani Kimetarjumiwa na: Hemedi Lubumba Selemani

Kimepangwa katika Kompyuta na: Ukhti Pili Rajab

Toleo la kwanza: Januari, 2014 Nakala: 1000 Kimetolewa na kuchapishwa na: Alitrah Foundation S.L.P. 19701 Dar es Salaam, Tanzania Simu: +255 22 2110640 Simu/Nukushi: +255 22 2127555 Barua Pepe: alitrah@yahoo.com Tovuti: www.ibn-tv.com Katika mtandao: www.alitrah.info



YALIYOMO Hukmu ya kusoma sura hizo ndani ya sala...............................2 Dalili za Rai ya Mahanafi..........................................................2 Rai ya madhehebu mengine na dalili zao juu ya hilo...............4 Rai ya Imamiya na dalili zao juu ya hilo..................................7 Muhtasari wa uchunguzi..........................................................21


NENO LA MCHAPISHAJI Kitabu kilichoko mikononi mwako ni tarjuma ya kitabu cha Kiarabu kiitwacho, Qira’atu ‘l-’Aza’im Fi ‘s-Swalah. Sisi tumekiita, Kusoma Sura zenye Sijda za Wajibu katika Sala. Kitabu hiki kimeshughulikia suala la usomaji wa sura ambazo ndani yake kuna aya za “sijda wajibu.” Kuna tofauti kati ya Shia na Sunni juu ya suala hili, na halikadhalika kuna tofauti ndani ya madhehebu za Sunni zenyewe. Wanazuoni wa Kiislamu kama kawaida ya wanadamu, wamehitilafiana katika hukumu ndogondogo katika matendo ya ibada, lakini kama ilivyo, tofauti ndogo kati ya wanazuoni kwa wafuasi inakuwa ni mlima wa tofauti na kusababisha zogo lisilo na maana. Mambo ambayo wanazuoni wetu wamehitilafiana si katika asili au misingi ya dini, na isitoshe ni mambo machache sana ukilinganisha na yale tunayokubaliana nayo. Tumekiona kitabu hiki ni chenye manufaa sana, hususan wakati huu wa maendeleo makubwa ya elimu katika nyanja zote, ambapo uwongo, ngano za kale na upotoshaji wa historia ni mambo ambayo hayana nafasi tena katika akili za watu.


Tunamshukuru ndugu yetu, Hemedi Lubumba Selemani kwa kukubali jukumu hili la kukitarjumi kitabu hiki. Vilevile tunawashukuru wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwake. Mchapishaji: Al-Itrah Foundation


NENO LA JUMUIYA Hakika mirathi ya Ahlul-Bait ambayo imehifadhiwa na kambi yao na wafuasi wao dhidi ya upotovu inaonyesha ni kambi iliyokusanya aina mbalimbali za taaluma za kiislamu. Kambi hii imeweza kulea nafsi mbalimbali zilizo tayari kunywa kutoka kwenye chemchemi hiyo, na kuupa umma wa kiislamu wanavyuoni wakubwa wenye kufuata nyayo za ujumbe wa AhlulBait. Wanavyuoni waliokusanya vidodosa na maswali mbalimbali ya madhehebu na mitazamo tofauti ya kifikira kuanzia ndani ya desturi ya kiislamu hadi nje ya desturi hiyo, huku wao wakitoa majibu na utatuzi makini juu ya maswali hayo ndani ya karne zote. Jumuiya ya kimataifa ya Ahlul-Bait imefanya hima kutetea utukufu wa ujumbe wa Uislamu na ukweli wake ambao umechafuliwa na makundi, madhehebu na wanaharakati mbalimbali wenye chuki na Uislamu. Jumuiya imefuata nyayo za Ahlul-Bait na za wafuasi wa kambi yao njema ambayo imefanya hima kujibu madai yenye kuendelea na daima ikijaribu kubaki ndani ya msitari wa mapambano kwa kiwango kinachohitajika ndani ya kila zama. Hakika uzoefu ambao umehifadhiwa ndani ya vitabu vya wanavyuuoni wa kambi ya Ahlul-Bait katika dhamira hii ni wa aina ya pekee, kwa sababu una akiba ya kielimu inayotegemea akili na hoja, huku ukijiepusha na matamanio na upendeleo uliokatazwa. Unazungumza na wasomi na wanafikra wenye fani maalumu,


mazungumzo ambayo yanakubalika kiakili na yanapokewa na maumbile yaliyo salama. Jaribio hili la Jumuiya ya kimataifa ya Ahlul-Bait limekuja kuwapa watafuta ukweli hatua mpya ya uzoefu wa thamani katika ulingo wa mazungumzo na maswali na kujibu hoja za utata zilizotolewa zama zilizopita au zinazotolewa leo kwa njia ya Tovuti, na hasa kwa kupewa nguvu na baadhi ya duru zenye chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu. Ikijiepusha na uchochezi uliokatazwa, na ni yenye kuhangaikia kuzishauri akili zenye kufikiria na nafsi zenye kutafuta haki, ili ziweze kufikia kwenye haki ambayo inatolewa na Kambi ya AhlulBayt ulimwengu mzima, ndani ya zama ambazo akili inaerevuka na nafsi na roho zinaboreka kwa kasi ya pekee. Ni lazima tugusie kuwa mfululizo huu wa tafiti hizi umeandaliwa na Kamati maalumu toka jopo la wanachuoni watukufu, hivyo tunatoa shukurani njema kwa hawa wote na kwa wasomi na wahakiki kwa kila mmoja miongoni mwao kwa kupitia sehemu ya tafiti hizi na kutoa mchango wao wa thamani kuhusu tafiti hizi. Na sote tunategemea na kutaraji kuwa tutakuwa tumetoa kile tulichokiweza katika juhudi za kutekeleza baadhi ya wajibu tulionao mbele ya ujumbe wa Mtukufu Mola Wetu Mlezi ambaye alimtuma Mtume Wake na uongofu na dini ya haki ili aipe ushindi dhidi ya dini zote. Na Mwenyezi Mungu anatosha kuwa shahidi.

Jumuiya ya kimataifa ya Ahlu-Bait Kitengo cha utamaduni



Kusoma Sura Zenye Sijda

HUKMU YA KUSOMA SURA HIZO NDANI YA SALA Nazo kwa mujibu wa Fiqhi ya kishia ni Sura As-Sajda, Fuswilat, AnNajmi na Al-A’laq. Na wala haijumuishi maeneo mengine ya Aya zilizo na sijda. Bila shaka madhehebu za kiislamu zimetofautiana kuhusu hukmu ya sijda itokanayo na kisomo, kwa yule aliyesoma moja ya Aya zilizo na sijda akiwa ndani ya Swala yake. Mahanafi wamesema: “Inajuzu kusoma, na aliye ndani ya Swala atakapoisoma ni wajibu kwake haraka sana kusujudu ndani ya Swala.” Madhehebu mengine yamesema: “Inaruhusiwa kuisoma ndani ya Swala lakini ni karaha kufanya hivyo. Na si wajibu kusujudu, kwani kwao wao haujathibiti wajibu wa sijda itokanayo na kisomo.” Imamiya wanasema: “Hairuhusiwi kusoma moja ya Sura hizo nne ndani ya Swala, na Swala hubatilika kwa hilo, kutokana na wajibu wa kusujudu uliyomo humo.” Uchambuzi huu umetengwa ili kudurusu rai hizi tatu na kubainisha dalili zake na hatimaye kuteua iliyo sahihi, ile inayoungwa mkono na dalili ya Kitabu na Sunna ya Mtukufu Mtume (s.a.w.w.).

DALILI ZA RAI YA MAHANAFI Abu Hanifa na wafuasi wake wametetea wajibu wa sijda ya kisomo kwa kutumia dalili mbalimbali, kati ya hizo ni kauli ya Allah: 2


Kusoma Sura Zenye Sijda

“Basi wana nini hawaamini. Na wanaposomewa Qur’ani hawasujudu.” (Surat Al-Inshiqaq: 20 - 21). Hapo akawalaumu kwa kuacha kwao kusujudu na akawakemea, na hilo likaonyesha wajibu wa kusujudu.1 Na kati ya hizo ni kauli ya Mtukufu Mtume (s.a.w.w.): “Sijda ni wajibu kwa aliyeisikia na kwa aliyeisoma.”2 Na kati ya riwaya hizo ni ile riwaya iliyopokewa na Abu Huraira kutoka kwa Mtukufu Mtume (s.a.w.w.), kuwa alisema: “Mwanadamu asomapo Aya ya sijda Shetani hujitenga huku akisema: ‘Ole wangu! Mwanadamu ameamriwa kusujudu na amesujudu, anapata pepo. Nami niliamriwa kusujudu nikakataa, ninapata moto.’” Amesema ndani ya kitabu Fat’hul-Qadiir: “Na asili ni kuwa mwenye hekima anaponukuu maneno ya asiyekuwa na hekima bila ya kuyakanusha, basi hilo huwa ni dalili ya usahihi wake. Hivyo Aya ni dhahiri kwenye wajibu, zaidi ya hapo ni kuwa Aya za sijda nazo zinaonyesha hivyo, kwa sababu zenyewe zina vifungu vitatu: Kifungu chenye amri iliyo wazi ikiamuru. Kifungu chenye hekaya ya jinsi makafiri walivyopinga, kwani waliamrishwa kufanya hivyo. Na kifungu kingine kina hekaya ya kitendo cha manabii walivyosujudu. Na vyote kuanzia kutekeleza amri, kuwafuata manabii na kuwapinga makafiri, ni wajibu, ila pale dalili itakapobainisha kuwa moja - kati ya 1. Sharhu Fathul-Qadiir cha Muhammad bin Abdul-Wahid Juz. 1, Uk. 465. Pia tazama Al-Mughniy cha Ibnu Qadamah Juz. 1, Uk. 652. Al-Wahiy AlKabiir Juz. 2, Uk. 200, chapa ya Darul-Kutub Al-Il’miyyah. 2. Sharhu Fathul-Qadiir cha Muhammad bin Abdul-Wahid Juz. 1, Uk. 466. 3


Kusoma Sura Zenye Sijda hivyo vitatu - si wajibu…..”3 Baada ya kuthibiti wajibu wake kwao, imekuwa kuutekeleza ni wajibu kwa kila anayeisoma Aya ya sijda, bila kuwepo tofauti baina ya yule anayekuwa katika hali ya Sala na nyingineyo. Sijda ya kisomo inapokuwa wajibu ndani ya Sala, kwao wao huchukua sifa ya Sala.4

RAI YA MADHEHEBU MENGINE, NA DALILI ZAO JUU YA HILO Madhehebu mengine ya kisunni yenyewe yameona kuwa sijda ya kisomo si wajibu, wakasema kuwa yenyewe ni mustahabu. Ibnu Qadamah amesema: “Hakika sijda ya kisomo ni Sunna iliyotiliwa mkazo, na wala si wajibu kwa imamu wetu, Malik, Al-Awzaiy, AlLaythi na Shafiy. Nayo ndio madhehebu ya Umar na mwanaye Abdullah.”5 Al-Mawridiy amesema: “Ni mustahabu kwa anayeisoma au kuisikia toka kwa anayeisoma, kusujudu kwa ajili yake, awapo ndani ya Sala au nje ya Swala. Na wala si wajibu kwake, sawa awe msomaji au msikiaji, na hii ndio kauli ya Umar na ndio madhehebu ya Malik.”6

3. Sharhu Fathul-Qadiir cha Muhammad bin Abdul-Wahid Juz. 1, Uk. 466, chapa ya Daru Ihyait-Turathil-Arabiy. 4. Sharhu Fathul-Qadiir cha Muhammad bin Abdul-Wahid Juz. 1, Uk. 470, chapa ya Daru Ihyait-Turathil-Arabiy. 5. Al-Mughniy Juz. 1, Uk. 652. 6. Al-Wahiy Al-Kabiir cha Ali bin Muhammad Al-Mawridiy Juz. 2, Uk. 200, chapa ya Darul-Kutub Al-Il’miyyah. 4


Kusoma Sura Zenye Sijda Na Ibnu Hazmi amesema mfano wa hayo ndani ya kitabu AlMahalliy.7 Ibnu Qadamah ametetea rai ya masunni wengi kwa kusema: “Na tunayo riwaya aliyoipokea Zayd bin Thabit, amesema: ‘Nilisoma (AnNajmi) kwa Mtume na hakusujudu yeyote yule miongoni mwetu.’Nayo inakubalika na kwa kuwa yenyewe ni ijmai ya sahaba. Bukhari na Al-Athram wamepokea kutoka kwa Umar kuwa alisoma siku ya Ijumaa akiwa juu ya mimbari Sura Nahli mpaka alipofika Aya ya sijda, akashuka akasujudu, na watu wakasujudu. Ilipowadia Ijumaa iliyofuata akaisoma tena mpaka alipofika Aya ya sijda, akasema: ‘Enyi watu! Hakika tunapita kwenye sijda, hivyo atakayesujudu atakuwa amepatia, na ambaye hatosujudu si dhambi kwake.’ Na Umar hakusujudu. Na katika lafudhi nyingine: “Hakika Allah hakutuwajibisha kusujudu ila tupendapo wenyewe.” Na katika riwaya ya Al-Athram: “Akasema: ‘Ni wajibu juu ya mitume wenu, hakika Allah hakuifaradhisha juu yetu ila tutakapo.’ Akaisoma wala hakusujudu na akawazuia kusujudu. Na hili lilikuwa mbele ya kundi kubwa na hakuna yeyote aliyekanusha wala kunukuu kinyume chake. Ama Aya, yenyewe imewalaumu wao kwa kuacha kusujudu kwa kule kutoamini ubora wake wala sheria yake, na kipimo chao kinatenguka kwa sijda ya sahau, kwani yenyewe kwao si wajibu.”8

7. Al-Mahalliy Juz. 5, Uk. 10, chapa ya Darul-Jayli. 8. Al-Mughniy Juz. 1 Uk. 652. 5


Kusoma Sura Zenye Sijda Al-Mawridiy ametetea kauli yake kwa kusema: “Dalili yetu ni riwaya ya Atau bin Yasar iliyopokewa kutoka kwa Zayd bin Thabit, kuwa alisoma Sura Najmi mbele ya Mtume wa Allah (s.a.w.w.) na hakusujudu. Hivyo lau kama ingekuwa ni wajibu basi Mtume wa Allah angesujudu na angemwamuru Zayd kufanya hivyo. Na imepokewa kuwa: Kuna mtu mmoja aliisoma Aya ya sijda mbele ya Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) kisha akasujudu, na akaisoma mwingine lakini yeye hakusujudu, Mtume akasema: ‘Ulikuwa imamu wetu, lau kama ungesujudu tungesujudu.’ Ndani ya kisa hicho kuna dalili mbili: Mojawapo: Hakika yeye hakumwamuru kusujudu na aliridhia kuiacha kwake. Ya pili: ‘Lau kama ungesujudu tungesujudu’ ipo katika hali ya hiari na kufuata hiari hiyo. Shafiy amepokea kuwa Umar bin Khattab alisoma Aya ya sijda juu ya mimbari siku ya Ijumaa, kisha akasujudu. Akaisoma tena Ijumaa iliyofuata, watu wakajiandaa kusujudu, akasema: “Enyi watu! Ni wajibu juu ya mitume wenu, hakika Allah hajaifaradhisha kwetu ila tutakapo.’ Pia Shafiy amepokea kutoka kwake kuwa alisema: “Atakayesujudu atakuwa amefanya jambo jema, na ambaye hatosujudu hana dhambi.” Hivyo kauli yake hii mbele ya hadhara ya kundi la muhajirina na answari, na wao kutompinga, ni dalili ya kuwa wao wamekubaliana kwa ijmai kuwa yenyewe si wajibu. Na kwa sababu katika baadhi ya hali sijda ni wajibu kutekelezwa na msafiri, hivyo ikalazimu isiwe wajibu kiasili kama ilivyo sijda ya Sunna. Na kwa kuwa yenyewe ni Swala isiyo ya wajibu, hivyo ikalazimu hata sijda yake kiasili isiwe wajibu iwapo utakariri kuisoma Aya hiyo. Na kwa kuwa sijda hiyo imekuwa si wajibu unapokariri kuisoma (Aya hiyo), imekuwa pia si wajibu uanzapo kuisoma, kama ilivyo tohara. Na kwa sababu kila sijda ambayo haibatilishi Sala kwa 6


Kusoma Sura Zenye Sijda kuiacha ni Sunna kama ilivyo sijda ya sahau. Ama kauli yake:

“Na wanaposomewa Qur’ani hawasujudu.” (Sura Al-Inshiqaq: 21). Muradi wake ni makafiri, kwa kule kufuatiwa na ahadi ya adhabu ambayo haimsitahiki yule aliyeacha sijda ya kisomo. Na kauli yake: “Hawasujudu.” Inamaanisha hawaitakidi, hivi huoni kauli yake: “Bali waliokufuru wanakanusha tu.” (Sura Al-Inshiqaq: 22). Ama kipimo chao, chenyewe ni batili kwa sijda ya sahau. Zaidi ya hapo ni kuwa maana ya sijda ya Swala ni ile iliyoratibiwa ndani ya nyakati maalumu.”9 Hii ndio rai yao katika asili ya sijda ya kisomo. Ama kusoma ndani ya Swala zile Aya za sijda zikiwemo Sura nne zenye Aya zilizo na sijda, ni jaizi kwao na hawana maneno katika hilo. Kisha wanatenganisha hukmu ya suala hilo kati ya Swala ya jamaa na ile ya mtu mmoja.

RAI YA IMAMIYA NA DALILI ZAO JUU YA HILO Imamiya wametoa dalili juu ya rai yao kuhusu mas’ala hii kwa kutumia dalili ambazo tutazinukuu kutoka kwenye vyanzo vyao maarufu, moja baada ya nyingine, baada ya kuondoa zile dalili zilizo mahsusi kwao, ambazo wametumia kuthibitisha hilo. Nazo ni riwaya zilizopokewa kutoka kwa Maimamu wa Ahlul-Bait (a.s.) kuhusu kadhia hii. 9. Al-Wahiy Al-Kabiir Juz. 2 Uk. 200 – 201. 7


Kusoma Sura Zenye Sijda As-Sayyid Al-Murtaza amesema katika kitabu Al-Intiswar: “Na kigezo cha kuzuia hilo ukiachia mbali ijmai iliyojikariri, ni kuwa kila moja kati ya Sura hizi ina sijda ya wajibu isiyo na shaka, hivyo akiisujudu atakuwa amezidisha (sijda) ndani ya Swala, na kama ataiacha atakuwa amevuruga wajibu.”10 Sheikh Tusy amesema ndani ya kitabu Al-Khilaaf kuhusu kutoruhusiwa kusoma Sura hizo ndani ya Swala: “Dalili yetu ni ijmai ya kundi letu na habari zao, na pia dhima yenye kushughulishwa na Swala kwa yakini, na wala haiondoki ila kwa yakini mfano wake, nayo ni kusoma Sura isiyo na Aya yenye sijda ya wajibu….”11 Na akathibitisha wajibu wa kufanya sijda katika Sura zenye Aya yenye sijda ya wajibu, kwa kutumia dalili mbalimbali, ya kwanza ni: “Ijmai ya kundi, hakika wao hawatofautiani kuhusu hilo.”12 Al-Alamah Al-Hilliy ametoa dalili ndani ya kitabu At-Tadhkirah juu ya kutoruhusiwa kusoma ndani ya Swala zile Sura zenye Aya zenye sijda ya wajibu, akasema: “……Na ni kwa kuwa sijda ya kisomo ni wajibu, na kuzidisha sijda kunabatilisha (Swala). Na Sunni wamekubaliana kuwa inajuzu kiasili. Na hakika inakuwa ni hoja lau kama tu hakijajitokeza kipingamizi.”13 Mwandishi wa kitabu Al-Jawahir ameongeza kusema: “Wajibu wa sijda ya kisomo unaweza kupatikana toka ndani ya kauli yake:

10. Al-Intiswar: 146. 11. Al-Khilaaf, Juz. 1, Uk. 426, chapa ya Jamaatul-Mudarrisiin- Qum. 12. Al-Khilaaf, Juz. 1, Uk. 431, chapa ya At-Tadhkirah, Juz. 3, Uk. 146. 13. Jamaatul-Mudarrisiin- Qum. 8


Kusoma Sura Zenye Sijda

“Na wanaposomewa Qur’ani hawasujudu.” (Sura Al-Inshiqaq: 21) Kwa kuzingatia kuwa ni lawama kwa kuacha kusujudu kwa ajili ya kisomo cha Qur’ani. Na baada ya ijmai na mengineyo haina sehemu ila Sura nne zilizotajwa zilizo mahsusi…”14 Ni wazi kuwa rai ya Imamiya imejengeka juu ya misingi miwili: Wa kwanza: Wajibu wa kusujudu pindi usomapo Aya yenye sijda katika Sura nne zenye Aya zilizo na sijda ya wajibu. Wa pili: Swala hubatilika kwa kule kuleta sijda kwa ajili ya Aya yenye sijda ya wajibu, kwa kuzingatia kuwa sijda hiyo ni ziada iliyo nje ya asili ya Swala. Na ni maalumu kuwa mukalafu analazimika kuitimiza Swala na kutoibatilisha kwa kuiletea kitendo cha nje pindi awamo ndani ya Swala, hivyo inalazimu kutokutenda mfano wa kitendo hicho, kwa kuwa chenyewe wakati huo kitakuwa ni miongoni mwa mifano halisi ya wazi kabisa yenye kupingana na lengo. Hivyo misingi yote hii miwili kwa pamoja inazaa hali ya kutokuruhusiwa kusoma Sura zenye Aya zenye sijda ya wajibu ndani ya Swala. Mahanafi wamewaafiki Imamiya katika msingi wa kwanza, huku wenyewe wakipanua wajibu hadi katika kila Aya yenye sijda ndani ya Qur’ani Tukufu. Na wamewakhalifu katika msingi wa pili, na masunni wengine wamewakhalifu katika misingi yote miwili. 14. Jawahirul-Kalaam, Juz. 10, Uk. 214, chapa ya Najaf Tukufu. 9


Kusoma Sura Zenye Sijda Licha ya kuwa masunni, kuanzia mahanafi hadi wengineo wametoa dalili mbali mbali tulizozitaja huko mwanzo juu ya kukhalifu kwao misingi hiyo miwili, ila ni kuwa uchunguzi wa kina wa kielimu unatuongoza kuamini utimilifu wa misingi hiyo miwili, na kutosihi kwa mjadala na upinzani uliotolewa juu yake. Ama kukhalifu kwao msingi wa kwanza ni kuwa wao wamedai kuwa sijda ya kisomo cha Sura hizo si wajibu, kwa mujibu wa dalili, nazo ni: Wamepinga kuwa Aya hii:

“Na wanaposomewa Qur’ani hawasujudu.” (Sura Al-Inshiqaq: 21) inaonyesha wajibu wa kusujudu. Riwaya ya Atau bin Yasar. Riwaya ya mtu mmoja aliyoipokea toka kwa Mtume (s.a.w.w.) kuhusu hilo.

wa Allah

Riwaya kutoka kwa Umar bin Khattab kuhusu hilo, inaonyesha ijmai ya sahaba juu ya kutowajibika kusujudu. Hakika kila sijda isiyobatilisha Sala kwa kuiacha ni Sunna. Hakika kule kutekeleza sijda ya kisomo ukiwa juu ya mnyama kwa msafiri anayeweza kuteremka kunaonyesha kuwa yenyewe ni mustahabu. Hizi ndio hoja na dalili ambazo wamezitumia kutetea kuwa sijda ya kisomo si wajibu, na sisi hapa tutazijadili ili tuone kiwango cha nguvu zake. 10


Kusoma Sura Zenye Sijda Ama kupinga kwao Aya kuonyesha wajibu ni madai yasiyo na hoja. Na pia ila ya upinzani wao kuwa msemezwa katika Aya ni makafiri, nayo pia si sahihi. Kwa sababu kipimo ni ule mjumuisho wa lafudhi na si sababu, kama wasemavyo wafasiri, na kuwa sababu haiifungi hukumu, kama wasemavyo wanataaluma wa misingi ya sheria, bali msemezwa katika Aya ni mjumuisho wa muumini na kafiri, hiyo ni kwa sababu kitu kilichokua maudhui yaliyopelekea Aya kushuka ni kule kutokusujudu kwa ajili ya jambo ambalo lenyewe tu lilivyo linastahiki sijda, bila kujali usadikisho na imani, nalo ni kisomo cha Qur’ani Tukufu. Na ni wazi kuwa ubaya wa hali hii unaongezeka pale inapokuwa kule kutokusujudu kunaambatana na ukanushaji wa kiburi, hivyo makafiri wakawa ndio wasemezwa wa mwanzo katika Aya, japokuwa msemezwa wake wa asili ni mjumuiko wa kafiri na muumini. Kwani ni wazi kuwa sijda haitekelezwi ila na muumini, na wala haiingii akilini Aya iwalaumu makafiri kwa kutokumsujudia Allah wakati wa kusoma kitabu Chake, ilihali wao bado wana hali ya ukafiri na ukinzani. Na hakika Aya imewalaumu wao (makafiri) kwa kutokusadiki kwao na kutoamini kwao Aya za Allah. Haistahiki kwa mwanadamu kuamini tu bali inastahiki kwake pia kusujudu pindi asomapo Aya hizo, hivyo Aya ilianza kulaumu kule kutoamini na ikamalizia kulaumu kule kutokusujudu:

“Basi wana nini hawaamini. Na wanaposomewa Qur’ani hawasujudu.” (Sura Al-Inshiqaq: 20 - 21). 11


Kusoma Sura Zenye Sijda Hivyo kinachotafutwa na Aya kutoka kwa makafiri ni imani, usadikisho na kukubali, kisha baada ya kuamini, kusadikisha na kukubali wanaombwa watekeleze amri mpya, nayo ni kusujudu pindi wasomapo Aya za Kitabu Kitukufu. Kama ilivyo amri kwa upande wa waumini wengine. Na kwa kuwa ijmai imesimama juu ya msingi wa kutokuwepo wajibu wa sijda kwa ajili ya kusoma Qur’ani Tukufu, hivyo ili kukusanya baina ya Aya na ijmai hii, inakuwa ni wajibu kusujudu wakati wa kusoma Aya mahsusi, nazo ni zile zenye maana ya amri ya kusujudu, hivyo Aya ikaonyesha kwa ukamilifu bila doa ule wajibu wa sijda ya kisomo. Ama riwaya ya Atau bin Yasar kutoka kwa Zayd bin Thabit, wameipokea Bukhari na Muslim katika Sahih zao. Na maelezo ya yake katika Bukhari ni kutoka kwa Ibnu Qusayt, kutoka kwa Atau bin Yasar, kuwa alimpa habari kuwa alimuuliza Zayd bin Thabit, akadai kuwa alisoma mbele ya Mtukufu Mtume: “Wan-Najmi” na hakusujudu.15 Na katika Sahih Muslim ni kutoka kwa Ibnu Qusayt, kutoka kwa Atau bin Yasar, kuwa alimpa habari kuwa alimuuliza Zayd bin Thabit kuhusu kusomwa na imamu, akasema: “Haina wajibu wowote wa kusomwa na imam.” Na akadai kuwa yeye alisoma kwa Mtume wa Allah: “Wan-Najmi” na hakusujudu.16 Ni kuwa riwaya inainukuu Sunna ya kitendo cha Mtume (s.a.w.w.), na kuna riwaya nyingine inatunukulia Sunna ya kitendo chake (s.a.w.w.) kikionyesha kuwa yeye alisujudu katika Sura An-Najmi. Riwaya hiyo kaipokea Abdullah bin Umar na ameitaja Bukhari katika Sahih yake 15. Sahih Bukhar Juz. 2 Uk. 32, chapa ya Darul-Fikr. 16. Sahih Muslim Juz. 2 Uk. 88, chapa ya Darul-Fikr. 12


Kusoma Sura Zenye Sijda kwenye mlango wenye jina “Mlango wa sijda ya Najmi.” 17 Maarufu ni kuwa Sunna ya kitendo ni fumbo huwa haitumiki kuthibitisha wajibu wala mustahabu, bali hutumika kuthibitisha ile hali ya kuthibiti jambo kisheria, (bila ya kujua hili lililothibiti kisheria ni mustahabu au ni wajibu). Kama ambavyo riwaya ya Abdullah nayo haionyeshi wajibu, kwani huenda kusujudu kwa Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) ilikuwa ni kwa ajili ya mustahabu. Kama ambavyo pia riwaya ya Atau bin Yasar haionyeshi kutokuwa wajibu, kwani huenda Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) alisujudu baada ya hapo, na hasa ukizingatia kuwa mpokezi ambaye ni Atau amenukuu jibu kutoka kwa Zayd bin Thabit, ambalo yeye (Atau) amelisifu kwa “Anadai”, neno ambalo hutumika kumaanisha maneno ambayo bado hayajathibitika, nayo ni sawa na madai matupu, na ni kama ndani ya nafsi ya Atau mna shaka dhidi ya maneno ya Zayd. Ama riwaya ya mtu ambaye Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) alimwambia: “Lau kama ungesujudu tungesujudu.” Aliyoyataja mwandishi wa kitabu Al-Hawiy Al-Kabiir, yenyewe haina nyororo ya wapokezi, hivyo haina mazingatio yoyote. Ama dai la ijmai ya sahaba kuhusu suala hili, ijmai iliyotokana na maneno ya Umar bin Khattab na kunyamaza kwa sahaba, iliyopokewa ndani ya Sahih Bukhar18 na Sunanul-Bayhaqiy19 , iwapo itasihi basi itahusu Aya mbili tu ‘49 na 50’ katika Sura Nahli. Kwa sababu ilivyotajwa ndani ya Sahih Bukhari ni kuwa Umar bin Khattab aliso17. Sahih Bukhari Juz. 2 Uk. 32, chapa ya Darul-Fikr. 18. Sahih Bukhari Juz. 2 Uk. 33 - 34, chapa ya Darul-Fikr. 19. Sunanul-Bayhaqiy Juz. 2 Uk. 320, milango ya sijda ya kisomo, mlango wa ambaye hajaona wajibu wa sijda ya kisomo. 13


Kusoma Sura Zenye Sijda ma Sura Nahli ndani ya Ijumaa mbili zilizotajwa, akasujudu katika Ijumaa ya kwanza na akakataza kusujudu katika Ijumaa ya pili, kwa sababu madhehebu yametofautiana kuhusu idadi ya maeneo yenye sijda ndani ya Qur’ani Tukufu. Kwa mujibu wa madhehebu ya AhlulBait si wajibu kusujudu kila sehemu ya Qur’ani iliyo na amri ya kusujudu au maana yake, bali kuna maeneo maalumu ambayo ndio wajibu kusujudu na si mengine. Na itikadi ya Ahlul-Bait ni kuwa sijda ni wajibu katika sehemu nne, nazo ni Aya zenye sijda zinazopatikana katika Sura As-Sajda, AnNajmi, Al-A’laq na Fuswilat. Hiyo ni kinyume na mahanafi ambao wanaona kuwa ni wajibu kusujudu katika kila sehemu yenye sijda ya kisomo katika Qur’ani, ambazo idadi yake kwao wao inafikia sehemu kumi na nne.20 Na ni mustahabu katika maeneo mengine ya sijda ya Qur’ani Tukufu, nayo ni moja ya maeneo mengine kumi, yakiwemo maeneo hayo yaliyotajwa ya Sura Nahli, hivyo ijmai hii ya sahaba haikatazi wajibu wa sijda ya Sura zenye Aya zilizo na sijda ya wajibu, bali inathibitisha kuwa katika sehemu hii ya Qur’ani Tukufu (Aya mbili za Sura Nahli), sijda ni mustahabu, nayo inaunga mkono madhehebu ya Ahlul-Bait. Ama kauli yao kuwa kila sijda ambayo haibatilishi Swala kwa kuiacha ni mustahabu, kauli hiyo ni sahihi katika sijda ya Swala. Na kitendo cha kuivusha hukmu hadi kwenye sijda ya kisomo ni kufanya ulinganisho (Qiyas), na ulinganisho ni batili kwa mujibu wa baadhi ya madhehebu ya kisunni, achia mbali Imamiya. Na wenye kusema ulinganisho ni sahihi wanaona kuwa kulinganisha sijda ya kisomo na sijda ya Swala ni ulinganisho batili.21 20. Al-Fiqhi Alal-Madhahib Al-Arbaa Wamdh’hab Ahlil-Bayti Juz. 1, Uk. 605. 21. Umdatul-Qariy Juz. 7, Uk. 96, chapa ya Darul-Fikr. 14


Kusoma Sura Zenye Sijda Ama kitendo cha msafiri kufanya sijda ya kisomo kwa kuashiria awapo juu ya mnyama, na kutokulazimika kuteremka kwa ajili yake, hakionyeshi mustahabu, kwani kila faradhi ina sifa zake mahsusi, hivyo hakuna kizuizi kwa sijda ya kisomo kuwa na sifa hii. Na lau kama maneno ya mpinzani yatasihi, basi itawajibika kusema kuwa Swala ya maiti ni mustahabu, kwani yenyewe haina sijda wala rukuu. Ama maneno ya Al-Mawridiy ambayo kasema: “Asili yake ni sijda ya Sunna, na ni kwa kuwa ni Swala isiyokuwa ya wajibu, hivyo imelazimu hata sijda yake isiwe wajibu kiasili iwapo atakariri kuisoma Aya hiyo, na kwa kuwa imekuwa si wajibu unapokariri kuisoma basi imekuwa si wajibu pia uanzapo kuisoma.” Haijafahamika ndani ya maneno yake maana yenye kuingia akilini wala hoja ipatikanayo. Hivi ni ipi maana ya kusema: Asili katika sijda ya kisomo ni sijda ya Sunna, na kuwa sijda ya Sunna ni Swala isiyo ya wajibu? Kisha Swala ya Sunna japokuwa yenyewe binafsi si wajibu lakini inapokosa nguzo zake kama vile sijda na rukuu huwa batili, na wakati huo huo haiitwi Swala hata isemwe kuwa sijda yake si wajibu. Hivyo ni lazima kuleta nguzo za Swala ili mukalafu alipwe thawabu juu ya hilo. Na yule asiyeleta nguzo yoyote miongoni mwa nguzo ni sawa na yule ambaye hajaileta Sunna yenyewe, hivyo yeye hana kosa kwa kuwa Sunna si wajibu, na si mwenye kupata thawabu kwa kuwa yupo kwenye hukmu ya mtu ambaye hajaleta Sunna yenyewe. Kisha nini maana ya kauli yake: “Atakapokariri kusoma Aya hiyo.”22 Kwani hakuna aliyesema kuwa sijda ya kisomo ni wajibu wakati wa 22. Al-Hawiy Al-Kabiir cha Al-Mawridiy Juz. 3, Uk. 201, kitabu cha Swala, mlango wa sifa ya Swala na idadi ya sijda za Qur’ani. 15


Kusoma Sura Zenye Sijda kuikariri Aya. Na kila anayesema wajibu au mustahabu anaona hilo ni wakati wa kusoma Aya, na hakuna anayesema kuwa hilo ni wakati wa kuikariri tu. Kwa maelezo haya zinabatilika zile dalili walizozitaja juu ya sijda ya kisomo, kuwa si wajibu. Na inathibiti kuwa Aya inaonyesha wajibu timilifu, na zaidi ya hapo ni kauli ya Uthman bin Affan ambayo kaipokea Bukhari akisema: “Hakika sijda ni juu ya mwenye kuisikia.”23 Na Ibnu Abu Shayba amepokea ndani ya kitabu chake Al-Musannaf24 kutoka kwa Ibnu Umar kuwa alisema: “Sijda ni juu ya mwenye kuisikia.” Na Al-Ayniy ameandika dalili nyingine juu ya wajibu wa sijda ya kisomo ndani ya ufafanuzi wake wa Sahih Bukhar, nayo ni ile aliyoipokea Ibnu Abu Shayba kutoka kwa Hafsa, kutoka kwa Hujjaj, kutoka kwa Ibrahim na Nafiu na Said bin Jubair, kuwa wao wamesema: “Atakayesikia Aya ya sijda ni juu yake kusujudu.” Na kutoka kwa Ibrahim kwa njia sahihi: “Mtu atakaposikia Aya ya sijda ilihali akiwa anaswali basi asujudu.” Na kutoka kwa As-Shaabiy: “Sahaba wa Abdullah walikuwa wasikiapo Aya ya sijda husujudu, sawa wawe ndani ya Swala au nje.” Shaabah amesema: “Nilimuuliza Hamada kuhusu mtu anayesali kisha akasikia Aya ya sijda, akasema: Asujudu. Na Al-Hakam alisema mfano wa hayo. Na ametusimulia Hashim: Alitupa habari Mughira kutoka kwa Ibrahim, kuwa alikuwa akisema: “Mwenye janaba akisikia Aya ya sijda akoge kisha aisome na kusujudu, na kama hawezi kusoma kwa ufasaha basi asome Aya nyingine, kisha asu23.Sahih Bukhari, Juz. 2 Uk. 33. 24. Al-Musannaf, cha Ibnu Abu Shayba Juz. 1, Uk. 457. 16


Kusoma Sura Zenye Sijda judu.” Na ametusimulia Ubaydullah bin Musa kutoka kwa Aban AlAttar, kutoka kwa Qatadah kutoka kwa Said bin Al-Musayyab kutoka kwa Ibrahim, kuhusu mwenye hedhi asikiapo Aya ya sijda, akasema: “Ataashiria kwa kichwa chake na aseme: ‘Ewe Allah nimesujudu kwa ajili Yako.’” Na kutoka kwa Hasan kuhusu mtu aliyesahau sijda mwanzoni mwa Swala yake na hakuikumbuka mpaka alipofika mwishoni mwa rakaa ya Swala yake, akasema: “Atasujudu sijda tatu.” Na kama hakuikumbuka mpaka alipomaliza Swala yake kabla ya kutoa salamu, akasema: “Atasujudu sijda moja maadamu tu hajazungumza, na kama atazungumza basi ataianza Sala mwanzo.” Na kutoka kwa Ibrahim: “Atakaposahau sijda basi aisujudu popote pale atakapoikumbuka ndani ya Swala yake.” Na Mujahid aliulizwa kuhusu mtu anayeshakia sijda ilihali akiwa ameketi, hajui ameshasujudu au la, mujahid akasema: “Ukitaka isujudu, na utakapomaliza Swala yako sujudu sijda mbili ilihali ukiwa umeketi. Na ukitaka usisujudu, na mwishoni mwa Swala yako sujudu sijda mbili ilihali ukiwa umeketi.”25 Haya ndio maneno yote kuhusu msingi wa kwanza. Ama msingi wa pili, ambao ni kubatilika Swala kwa sijda ya kisomo, hilo ni kati ya mambo yaliyo wazi kabisa, kwa sababu mukalafu amejituma yeye mwenyewe kwa hiari yake kufanya sijda hii ndani ya Swala, kwa ajili ya kusoma kwake moja ya sura hizo ndani ya Swala, hivyo ameleta jambo lililo nje ya asili ya Swala, na tayari wanazuoni wa sheria ya kiislamu wamesema kuwa, Sala hubatilika kwa kule kuiwekea amali nyingi. 25. Umdatul-Qariy Juz. 7 Uk. 95, chapa ya Darul-Fikr. 17


Kusoma Sura Zenye Sijda Al-Jazairiy amesema ndani ya kitabu Al-Fiqhi Ala Madhahib AlArbaa kuwa: “Swala hubatilika kwa kuiwekea amali nyingi ambazo si katika jinsia ya Swala, nazo ni zile zinazomfanya mtazamaji aone kuwa mtendaji wake hayumo ndani ya Swala…..Ama mwenye kusali atakapotenda amali ya ziada iliyo nje ya jinsia ya Swala, kama vile kuzidisha rukuu au sijda, basi ikiwa ni kwa kukusudia, kichache au kingi, vyote hubatilisha. Na kama ni kwa kusahau basi Swala yake haibatiliki kwa namna yoyote ile.”26 Kwa ajili hiyo Shafiy amesema: “Mwenye kuswali atakaposoma Aya za sijda ndani ya Swala, na akawa kwa sijda hiyo anakusudia sijda ya kisomo, Swala yake imebatilika.”27 Kauli hiyo inakaribiana na kauli ya Imamiya. As-Sayyid Muhammad Kadhim Al-Yazdiy (r.a.) amesema ndani ya kitabu Al-Ur’watu AlWuthqa: “Hairuhusiwi kusoma moja ya Sura zenye Aya zilizo na sijda ya wajibu ndani ya Swala ya faradhi, na lau kama ataisoma makusudi, basi atalazimika kuianza upya Swala.”28 Hayo yote ni kuachia mbali tofauti iliyopo kati ya kauli mbili upande wa mambo mawili: Upande wa kwanza wa tofauti iliyopo ni kuwa, mashafi wanahukumu ubatilifu wa Swala kwa aliyesoma Aya ya sijda huku akikusudia kufanya sijda ya kisomo, ilihali wanafiqhi wa Imamiyya wao wanahukumu ubatilifu wa Swala kwa yule aliyesoma moja ya Sura hizo kwa makusudi, yaani ambaye hajasahau na wala si jahili wa hukmu yake, bali ni mjuzi mwenye kumbukumbu, hata kama atakuwa hajakusudia kufanya sijda ya kisomo. 26. Al-Fiqhi Alal-Madhahib Al-Arbaa Wamdh’hab Ahlil-Bayti Juz. 1 Uk. 430. Al-Fiqhi Alal-Madhahib Al-Khamsa cha Sheikh Muhammad Jawad Mughniyah: 145. 27. Al-Fiqhi Alal-Madhahib Al-Arbaa Wamdh’hab Ahlil-Bayti Juz. 1, Uk. 602. 28. Al-Ur’watul-Wuthqa Juz. 1, Uk. 644, Faslu ya 24 kuhusu kisomo. 18


Kusoma Sura Zenye Sijda Na upande wa pili wa tofauti ni kuwa mashafi wanahukumu ubatilifu wa Swala kwa yule aliyesujudu sijda ya kisomo hivi sasa, ama yule ambaye hajasujudu hana tatizo lolote. Wanaafikiana na Imamiya katika kuhukumu usahihi wa Swala katika sura kama hii, lakini wao (Imamiyya) wanamwona mtu huyo kuwa ni mwasi, na wanahukumu kuwa anatakiwa kurudia Swala kwa ajili ya tahadhari (ihtiyat) ya wajibu, kwa mujibu wa baadhi,29 na tahadhari (ihtiyat) ya Sunna kwa mujibu wa wengine.30 Na kinashangaza sana kitendo cha mahanafi kukhalifu katika kifungu hiki, kwa sababu yule atakayesoma Aya ya sijda ndani ya Swala atakuwa yeye mwenyewe amejiweka kati ya mambo mawili yenye kugongana. La kwanza: Wajibu wa kutimiza Swala na kutoruhusiwa kuibatilisha. La pili: Wajibu wa kufanya sijda ya kisomo haraka iwezekanavyo ndani ya Swala. Ukichukua kukiri kwa mahanafi kuwa sijda ya kisomo ni wajibu, basi vipi tena inakubalika kwao kusema kuwa, inaruhusiwa kusoma Aya ya sijda, ambayo matokeo yake ya lazima yanapelekea kubatilisha Sala? Je hii si kumpa ujasiri mwenye kusali abatilishe Sala yake? Je mwenye kusali si kaamriwa kutokubatilisha Sala yake? Kuifanyia kazi kauli hii kunapelekea kuwapo mgongano katika hukmu za kisheria, jambo ambalo linaonyesha kuwepo dosari kwenye msimamo huo wa kisheria. Na ni wazi kuwa mgongano huu haukomei kwenye Fiqhi ya mahanafi tu, wanaotoa fatwa ya wajibu wa kufanya sijda ya kisomo ndani ya Swala, bali inahusu hata mad29. Minhajus-Salihiin cha As-Sayyid Al-Khui Juz. 1 Uk. 164. 30. Minhajus-Salihiin cha As-Sayyid Sistaniy Juz. 1 Uk. 206. 19


Kusoma Sura Zenye Sijda hehebu mengine ya kisunni, wale wanaoamini kuwa inajuzu kufanya sijda ya kisomo ndani ya Sala, ijapokuwa fiqhi ya mahanafi inachukua daraja la juu kabisa. Kwa sababu kusema inajuzu sijda ya kisomo ndani ya Sala, inamaanisha sheria imekataza sijda ya kisomo kwa kigezo kuwa yenyewe ni ziada iliyo nje ya asili ya Swala, na kuwa yenyewe (sheria) wakati huohuo imeruhusu kuitekeleza ndani ya Swala. Upuuzi huu unafichua dosari za msimamo wa kifiqhi zilizopelekea kuficha kwa ndani mfano wa matokeo kama haya, na kisha kuyanasibisha na sheria. Imam (a.s.) alielezea uhalisia wa sheria pindi Zarara alipotoa habari toka kwa Imam Al-Baqir au As-Sadiq, kuwa mmoja wao alisema: “Msisome yoyote ile kati ya Sura zenye Aya zilizo na sijda ya wajibu ndani ya Swala ya faradhi, kwani kwa hakika sijda ni kuleta ziada katika Sala ya faradhi.�31

31. Al-Wasailu Juz. 4 Uk. 779, mlango wa 40 kati ya milango ya kisomo,hadithi ya 1. 20


Kusoma Sura Zenye Sijda

MUHTASARI WA UCHUNGUZI Kwa muhtasari ni kuwa maoni kuhusu suala la sijda ya kisomo ni matatu: Kauli isemayo inajuzu kusoma Aya ya sijda ndani ya Swala, na ni wajibu kusujudu kwa ajili ya kisomo, nayo ni kauli ya mahanafi. Kauli isemayo inajuzu kusoma na inajuzu kusujudu kwa ajili ya kisomo, nayo ni kauli ya madhehebu mengine ya kisunni. Kauli isemayo hairuhusiwi kusoma Sura nne zilizotajwa huko nyuma, na kuzisoma kunabatilisha Sala, nayo ni kauli ya Imamiya. Na iko wazi kuwa kauli ya Imamiya inategemea misingi miwili: Wa kwanza: Wajibu wa kusujudu kwa ajili ya kusoma Sura hizo. Na kutokana na uchambuzi huo tayari utimilifu wake umeshakuwa wazi. Mjadala na hoja zote zilizotolewa dhidi yake zimethibitika kuwa si sahihi. Wa pili: Swala hubatilika kwa kule kuleta sijda ya kisomo ndani ya Swala, na kuwa mukalafu atajiweka yeye mwenyewe kati ya mambo mawili yenye kugongana: Uharamu wa kubatilisha Swala na wajibu wa kuleta sijda ya kisomo itakayopelekea Swala yake kubatilika. Kwa ajili hiyo inalazimu kusema ni haramu kusoma moja ya Sura zenye Aya zilizo na sijda ya wajibu uwapo ndani ya Swala.

21


Kusoma Sura Zenye Sijda

ORODHA YA VITABU VILIVYO CHAPISHWA NA AL-ITRAH FOUNDATION 1. 2. 3. 4. 5. 6. 7. 8. 9. 10. 11. 12. 13. 14. 15. 16. 17. 18. 19. 20. 21. 22. 23.

Qur'an Al-Kariim - Tafsir Al-Kashif Juzuu ya kwanza mpaka Thelathini Uharamisho wa Riba Uharamisho wa uwongo Juzuu ya Kwanza Uharamisho wa uwongo Juzuu ya Pili Hekaya za Bahlul Muhanga wa Imamu Husein (A.S.) Mikingamo iliyomzunguka Imamu Ali (A.S.) Hijab vazi Bora Ukweli wa Shia Ithnaashari Madhambi Makuu Mbingu imenikirimu Abdallah Ibn Saba Khadijatul Kubra Utumwa Umakini katika Swala Misingi ya Maarifa Kanuni za Ndoa na maadili ya Familia Bilal wa Afrika Abudharr Usahihi wa Historia ya Uislamu na Waislamu Salman Farsi Ammar Yasir Qur'an na Hadithi 22


Kusoma Sura Zenye Sijda 24. 25. 26. 27. 28. 29. 30. 31. 32. 33. 34. 35. 36. 37. 38. 39 40. 41. 42. 43. 44. 45. 46. 47. 48. 49. 50. 51.

Elimu ya Nafsi Yajue Madhehebu ya Shia Ukusanyaji na Uhifadhi wa Qur'an Tukufu Al-Wahda Ponyo kutoka katika Qur'an. Uislamu mfumo kamili wa maisha ya kijamii Mashukio ya Akhera Al Amali Dua Indal Ahlul Bayt Udhuu kwa mujibu wa Kitabu na Sunna. Haki za wanawake katika Uislamu Mwenyeezi Mungu na sifa zake Kumswalia Mtume (s) Nafasi za Ahlul Bayt (a.s) Adhana. Upendo katika Ukristo na Uislamu Tiba ya Maradhi ya Kimaadili Maana ya laana na kutukana katika Qur'ani Tukufu Kupaka juu ya khofu Kukusanya swala mbili Bismillah ni sehemu ya Qur'ani na husomwa kwa Jahara Kuwaongoza vijana wa kizazi kipya Kusujudu juu ya udongo Kusherehekea Maulidi Ya Mtume (s) Tarawehe Malumbano baina ya Sunni na Shia Kupunguza Swala safarini Kufungua safarini 23


Kusoma Sura Zenye Sijda 52. 53. 54. 55. 56. 57. 58. 59. 60. 61. 62. 63. 64. 65. 66. 67. 68. 69. 70. 71. 72. 73. 74. 75. 76. 77.

Umaasumu wa Manabii Qur'an inatoa changamoto as-Salaatu Khayrun Mina -'n Nawm Uadilifu wa Masahaba Dua e Kumayl Sauti Ya Uadilifu wa Binadamu Umaasumu wa Mitume - Faida Zake Na Lengo Lake Umaasumu wa Mitume - Majibu Ya Aya Zenye Utata Umaasumu wa Mitume - Umaasumu wa Mtume Muhammad (s) Nahju'l-Balaghah - Juzuu ya Kwanza Nahju'l-Balaghah - Juzuu ya Pili Kuzuru Makaburi Maswali Na Mishkili Elfu - Sehemu ya Kwanza Maswali Na Mishkili Elfu - Sehemu ya Pili Maswali Na Mishkili Elfu - Sehemu ya Tatu Maswali Na Mishkili Elfu - Sehemu ya Nne Maswali Na Mishkili Elfu - Sehemu ya Tano Maswali Na Mishkili Elfu - Sehemu ya Sita Tujifunze Misingi Ya Dini Sala ni Nguzo ya Dini Mikesha Ya Peshawar Malezi Ya Mtoto Katika Uislamu Ubora wa Imam 'Ali Juu ya Maswahaba Na Ushia ndio njia iliyonyooka Hukumu za Kifikihi zinazowahusu Wanawake Liqaa-u-llaah Muhammad (s) Mtume wa Allah 24


Kusoma Sura Zenye Sijda 78. 79. 80. 81. 82. 83. 84. 85. 86. 87. 88. 89. 90. 91. 92. 93. 94. 95. 96. 97. 98. 99. 100. 101. 102 103. 104. 105.

Amani na Jihadi Katika Uislamu Uislamu Ulienea Vipi? Uadilifu, Amani na Mtume Muhammad (s) Mitala na Ndoa za Mtume Muhammad (s) Urejeo (al-Raja'a ) Mazingira Utokezo (al - Badau) Hukumu ya kujenga juu ya makaburi Swala ya maiti na kumlilia maiti Uislamu na Uwingi wa Dini Mtoto mwema Adabu za Sokoni Johari za hekima kwa vijana Maalimul Madrasatain Sehemu ya Kwanza Maalimul Madrasatain Sehemu ya Pili Maalimul Madrasatain Sehemu ya Tatu Tawasali Imam Mahdi katika Usunni na Ushia Hukumu za Mgonjwa Sadaka yenye kuendelea Msahafu wa Imam Ali Ngano ya kwamba Qur'ani imebadilishwa Idil Ghadiri Kusoma sura zenye Sijda ya wajibu Hukumu zinazomuhusu mkuu wa kazi na Mfanyakazi Huduma ya Afya katika Uislamu Sunan an-Nabii Historia na sera ya viongozi wema (Sehemu ya Kwanza) 25


Kusoma Sura Zenye Sijda 106. 107. 108. 109. 110. 111. 112. 113. 114. 115. 116. 117. 118. 119. 120. 121. 122. 123. 124. 125. 126. 127. 128. 129. 130. 131.

Historia na sera ya viongozi wema (Sehemu ya Pili) Shahiid Mfiadini Kumswalia Nabii (s.a.w) Ujumbe - Sehemu ya Kwanza Ujumbe - Sehemu ya Pili Ujumbe - Sehemu ya Tatu Ujumbe - Sehemu ya Nne Mariamu, Yesu na Ukristo kwa mtazamo wa Kiislamu Hadithi ya Thaqalain Maarifa ya Kiislamu Ukweli uliopotea sehemu ya Kwanza Ukweli uliopotea sehemu ya Pili Ukweli uliopotea sehemu ya Tatu Ukweli uliopotea sehemu ya Nne Ukweli uliopotea sehemu ya Tano Safari ya kuifuata Nuru Fatima al-Zahra Myahudi wa Kimataifa Kuanzia ndoa hadi kuwa Wazazi Visa vya kweli sehemu ya Kwanza Visa vya kweli sehemu ya Pili Muhadhara wa Maulamaa Mwanadamu na Mustakabali wake Imam Ali ('a) Ndugu wa Mtume Muhammad (s) (Sehemu ya Kwanza) Imam Ali ('a) Ndugu wa Mtume Muhammad (s) (Sehemu ya Pili) Khairul Bariyyah 26


Kusoma Sura Zenye Sijda 132. 133. 134. 135. 136. 137. 138. 139. 140. 141. 142. 143. 144. 145. 146. 147. 148. 149. 150. 151. 152 153. 154. 155. 156. 157. 158.

Uislamu na mafunzo ya kimalezi Vijana ni Hazina ya Uislamu. Yafaayo kijamii Tabaruku Taqiyya Vikao vya furaha Shia asema haya Sunni asema haya Wewe wasemaje? Visa vya wachamungu Falsafa ya Dini Kuhuzunika na Kuomboleza - Azadari Sunna katika Kitabu Fiqhi al-Sunnah Mtazamo Mpya - Wanawake katika Uislamu Kuonekana kwa Allah Tabia njema kwa Mujibu wa Ahlul-Bayt (Sehemu ya Kwanza) Tabia njema kwa Mujibu wa Ahlul-Bayt (Sehemu ya Pili) Ndugu na Jirani Ushia ndani ya Usunni Maswali na Majibu Mafunzo ya hukmu za ibada Ahlul Bayt ndani ya tafsiri za Kisunni No 1 Ahlul Bayt ndani ya tafsiri za Kisunni No 2 Ahlul Bayt ndani ya tafsiri za Kisunni No 3 Abu Huraira Vipengee kadhaa katika Swala ya Jamaa na Msikiti. Mazingatio kutoka katika Qur'an - Sehemu ya Kwanza Mazingatio kutoka kaitka Qur'an - Sehemu ya Pili Mazingatio kutoka katika Uislamu - Sehemu ya kwanza 27


Kusoma Sura Zenye Sijda 159. 160. 161. 162. 163. 164. 165. 166. 167. 168. 169. 170. 171. 172. 173. 174. 175. 176. 177. 178. 179. 180. 181. 182. 183. 184. 185.

Mazingatio kutoka katika Uislamu - Sehemu ya Pili Qur'ani Tukufu - Pamoja na Tarjuma ya Kiswahili Falsafa ya Mageuzi ya Imam Husein (a.s) Amali za Mwezi Mtukufu wa Ramadhani Elimu ya Tiba za Kiislamu - Matibabu ya Maimamu Uislamu Safi Majlisi za Imam Husein Majumbani Mshumaa Uislam wa Shia Amali za Makka Amali za Madina Asili ya Madhehebu katika Uislamu Sira ya Imam Ali kuhusu Waasi Ukweli uliofichika katika neno la Allah Uislamu na Mifumo ya Uchumi Umoja wa Kiislamu na Furaha Mas'ala ya Kifiqhi Jifunze kusoma Qur'ani As-Sahifatul Kamilah as-Sajjadiyyah Hayya 'Alaa Khayri'l-'Amal Katika Adhana Ukweli kuhusu Funga ya Siku ya Ashura Dua za Miezi Mitatu Mitukufu (Rajabu, Shaabani na Ramadhani) Uadilifu katika Uislamu Mahdi katika Sunna Jihadi ya Imam Hussein ('as) Kazi na Bidii ni njia ya maendeleo Abu Talib - Jabali Imara la Imani


Kusoma Sura Zenye Sijda 186. 187. 188. 189. 190. 191. 192. 193. 194. 195. 196. 197. 198. 199. 200. 201.

Ujenzi na Utakaso wa Nafsi Vijana na Matarajio ya Baadaye Usalafi - Historia yake, maana yake na lengo lake Ushia - Hoja na Majibu Mateso ya Dhuria wa Mtume (saww) Maombolezo - Msiba wa Bwana wa Mashahidi (a.s.) Shahidi kwa Ajili ya Ubinadamu Takwa Amirul Muuminina ('as) na Makhalifa Utawala na Uendeshaji katika Sera ya Imam Ali (a.s.) Kuelewa Rehma ya Mwenyezi Mungu Mtazamo kuhusu msuguano wa kimadhehebu Upotoshaji Dhahiri katika Turathi (Hazina) ya Kiislamu Nchi na Uraia - Haki na wajibu kwa Taifa Mtazamo wa Ibn Taymiyyah kwa Imam Ali (a.s.) Uongozi wa kidini - Maelekezo na utekelezaji wa Kijamii

KOPI NNE ZIFUATAZO ZIMETAFSIRIWA KWA LUGHA KINYARWANDA 1. 2. 3. 4.

Amateka Na Aba'Khalifa Nyuma yaho naje kuyoboka Amavu n'amavuko by'ubushiya Shiya na Hadithi

29


Kusoma Sura Zenye Sijda

BACK COVER Kitabu hiki kimeshughulikia suala la usomaji wa sura ambazo ndani yake kuna aya za “sijda wajibu.” Kuna tofauti kati ya Shia na Sunni juu ya suala hili, na halikadhalika kuna tofauti ndani ya madhehebu za Sunni zenyewe. Wanazouni wa Kiislamu kama kawaida ya wanadamu, wamehitilafiana katika hukumu ndogondogo katika matendo ya ibada, lakini kama ilivyo, tofauti ndogo kati ya wanazuoni kwa wafuasi inakuwa ni mlima wa tofauti na kusababisha zogo lisilo na maana. Mambo ambayo wanazuoni wetu wamehitilafiana si katika asili au misingi ya dini, na isitoshe ni mambo machache sana ukilinganisha na yale tunayokubaliana nayo. Ili kupata ufafanuzi wa suala hili, ungana na jopo la wanazuoni ambao wamelichambua suala hili kwa uzuri sana kwa kutumia vyanzo sahihi vya Kiislamu ambavyo ni Qur’ani na Sunna. Kimetolewa na kuchapishwa na: Alitrah Foundation S.L.P. 19701 Dar es Salaam, Tanzania Simu: +255 2110640 / 2127555 Barua Pepe: alitrah@yahoo.com Tovuti: www.ibn-tv.com Katika mtandao: www.alitrah.info

30


Turn static files into dynamic content formats.

Create a flipbook
Issuu converts static files into: digital portfolios, online yearbooks, online catalogs, digital photo albums and more. Sign up and create your flipbook.